Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Tulia Ackson Mwansasu amesema hakuna Mbunge ambaye ana hadhi ya juu kuliko mwingine katika Bunge, bali katiba inawatambua wabunge wote wapo sawa.
Akizungumza katika mahojiano maalumu katika kipindi cha dakika 45 kinachorushwa na kituo cha ITV, Naibu Spika amesema makundi yote ya wabunge yakishaapishwa wote ni wabunge wanaofanana katika hadhi ya kufanya kazi wanapokuwa Bungeni.
“Katiba ilivyoyaweka makundi matano ya wabunge kuanzia wanaoteuliwa na Rais, wanaochaguliwa na wananchi, wabunge wa viti maalum na wanaotoka Baraza la Wawakilishi Zanzibar na Mwanasheria Mkuu wa Serikali wote wamewekwa kwa sababu maalumu kwa sababu hiyo wabunge wote ni sawa” Amesema Dkt. Tulia Aidha Naibu Spika ameitaka jamii kubadilika kutoka katika dhana kwamba mwanamke ambaye anashika nafasi ya juu katika uongozi kwamba amebebwa.
“Wanawake wengi ambao wamepewa nafasi ya uongozi kwa kuchaguliwa au kuteuliwa ni mara chache sana hufanya vibaya na hata akifanya vibaya jamii humhukumu kwa kuwa ni mwanamke wakati kuna wanaume katika nafasi kama hiyo ambao pia unakuta wamefanya vibaya hivyo kuna changamoto hiyo katika jamii”
Amesema Naibu Spika Dkt. Tulia. Kwa upande mwingine Naibu Spika Dkt. Tulia amesema anaongoza Bunge bila upendeleo wowote ila anafuata sheria na kanuni za kuongoza Bunge.
No comments:
Post a Comment