Friday, June 10, 2016

ALBINO 400 WAUAWA NCHINI KWA MIAKA 12

  Shinyanga. Zaidi ya watu 400 wenye ulemavu wa ngozi (albino) wameuawa katika kipindi cha miaka 12 iliyopita kuanzia mwaka 2004.

  Akizungumza na waumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) mjini Shinyanga, Msemaji wa asasi isiyo ya kiserikali ya JT Foundation, Josephat Torner alisema mauaji hayo ni yale yaliyoripotiwa.

  Alisema siyo rahisi kumjua adui yako katika jamii tunayoishi hivyo hakuna budi kuendelea kukemea mauaji na kuhubiri amani. Aliwataka Wakristo kuwa na upendo ili kuhakikisha wanakomesha vitendo hivyo vinavyofanywa na watu wachache kwa imani potofu.

   “Tumeamua kupita kwenye nyumba za ibada kuhamasisha waumini na viongozi ili wakemee na kulaani mauaji ya ndugu zetu, pia tukumbuke kuwa vita hii haijulikani,”alisema Torner. Mchungaji wa kanisa hilo, Michael Lyimo aliitaka jamii kuwa na moyo wa upendo kwani vyote vilivyomo duniani ni mali ya bwana Yesu na kwamba Mungu anachukizwa na uovu.

  Waumini wa kanisa hilo, Tabu Alphonce na Shayo Moses walisema kukosekana kwa hofu ya Mungu miongoni mwa wanadamu ndicho chanzo cha maovu yote yakiwamo mauaji ya watu hao.

No comments:

Post a Comment